Hotuba ya Dkt. Hamisi Kigwangalla (MB), Mwenyekiti wa TAMISEMI Alipotangaza Nia Kugombea Urais 2015

Sunday, September 7, 2014

Hotuba Aliyoitoa Dkt. Hamisi Kigwangalla, MB (Nzega), Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya TAMISEMI, kwa Waandishi wa Habari Kutangaza Nia ya Kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mwaka 2015 Kwenye Ukumbi wa Zanzibar, Hyatt Regency, The Kilimanjaro Hotel, Dar es salaam, Siku ya Tarehe 7 Septemba 2014.


Utangulizi


Ndugu viongozi mlioko hapa, wazazi wangu, wageni waalikwa, wanahabari, marafiki zangu, mke wangu na watoto wangu,

Nianze kwa kuwashukuru viongozi wa dini kwa dua za utangulizi.

Pia nitume salamu zangu za rambirambi kwa Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mara, Eng. Evarist Ndikilo na ndugu, jamaa na marafiki wa watu waliopoteza maisha kutokana na ajali mbaya ya gari iliyotokea juzi. Pia nitumie fursa hii kutuma salamu zangu za rambi rambi kwa Inspekta Mkuu wa Jeshi la polisi, IGP Ernest Mangu, ndugu wa marehemu na askari wote wa jeshi la polisi kutokana na uvamizi wa kituo cha polisi kule Bukombe. Na pia naomba nitumie fursa hii kumpa pole Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar na Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi, CUF, Maalim Seif Sharif Hamad kwa kupata ajali eneo la Misungwi, Mwanza.

Ndugu zangu mlioko hapa, ni heshima na furaha kubwa sana kwangu kupata fursa hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezimungu kwa kutujaalia uhai na kutukutanisha hapa siku ya leo. Pili niwashukuru nyote mliofika hapa kuja kunisikiliza. Niwashukuru zaidi waandaaji wa Mkutano huu kwa kujitoa na kwa namna ya kipekee niwashukuru wazazi wangu, mke wangu na wanangu Sheila, Hawa na HK Jr kwa uvumilivu na kwa kuendelea kunitia nguvu ya kusonga mbele.

Leo nitasema neno zito kidogo, kama nilivyoahidi siku chache zilizopita. Neno nitakalolisema hapa litabadilisha sura ya historia yangu milele. Ninawashukuru nyote kwa kuitikia wito wa kuja kuwa mashuhuda wa namna historia itakavyoendelea kuandikwa hapa.

Kinachotokea hapa leo hii kina maana kubwa sana kwa watu wenye historia inayofanana na mimi. Wale ambao wameyajua maisha ya shida na kukosa uhakika toka wakiwa tumboni mwa wazazi wao kutokana na hali za uchumi wao. Wale wenzangu na mie ambao kesho yao haina uhakika; wale ambao wengine hupenda kuwaita ‘wanyonge’, ambapo mimi nikijitazama nilikotoka husema, hapana, hawa si wanyonge bali ni ‘simba aliyelala.’

Shukrani Kwa Urithi Toka kwa Waasisi na Wazee Walionitangulia


Mimi ninayezungumza hapa nimeyajua maisha ya mtu mnyonge na maskini kwa kuyaishi na si kwa kusoma ama kusikia. Ninajua mtu akiongelea njaa anamaanisha nini, sihitaji kufundishwa, najua. Nasema haya maana naujua ugumu wa kumuelewesha mtu anayekula milo mitatu kwa siku, tena ya kujipakulia kuwa kuna wengine wanakula pilau sikukuu hadi sikukuu. Ni ngumu sana kumuelewesha mtu wa aina hiyo kuwa wapo watoto wanaogombania chakula kwenye sahani moja. Maana kila siku yeye huwashuhudia watu wa dunia anayoishi wakihangaika kutembea umbali mrefu ili wapunguze vitambi na wakae kwenye ‘shape’ na hajui kama kuna watu wanatembea umbali mrefu ili kutafuta chakula wasukume siku!

Ni katika nchi chache sana duniani, mtoto mwenye historia ya maisha kama yangu, aliyewahi kutembea mitaani akiuza karanga, Big G, maandazi na jerebi ili kusaidia wazazi kupata chochote kwa ajili ya kulisha familia anaweza kuota ndoto ya kuwa Rais wa nchi yake. Kwamba, mtoto aliyeenda shule bila viatu anaweza kuwa Daktari.

Hii inamaanisha jambo moja kubwa, kwamba misingi ya haki na usawa kwa wote iliyowekwa na waasisi wa Taifa letu haikuwa ndoto za alinacha, bali ukweli na uhalisia, na inafanya kazi. Kwamba, siyo lazima uwe mtoto wa tajiri ama wa kiongozi, ndiyo uoneshe kipaji chako. Inadhihirisha kwamba, ukipigana ndani ya Tanzania unafanikiwa!

Hili peke yake linanipa sababu ya ziada ya kwa nini nitamani kusonga mbele zaidi – nataka niwe mfano hai wa mafanikio ya Ndoto ya waasisi wa Taifa letu, kuwa sote ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tuna haki na fursa sawa bila kujali nani anatokea familia ipi. Hii ni Tanzania ya ndoto za waliotutangulia. Ni lazima atokee kiongozi wa kizazi hiki anayetamani kuiongoza Tanzania itakayodumu kwenye misingi hii. Kwamba, ndani ya Tanzania, si lazima mtoto wa mama ntilie awe ‘baba-ntilie’ – anaweza kuwa mmiliki wa hoteli kubwa ya kitalii!

Kwa namna ya kipekee nichukue fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza waasisi wa Taifa letu kwa kuzilinda tunu hizi, maana ninaamini kuwa hatuwezi kuizungumzia kesho bila kukumbuka shida na raha tulizopata jana.

Leo nimefika hapa kwa sababu chama changu kina mfumo mzuri ulioasisiwa na Mwl. Nyerere na umelindwa na wenyeviti waliomfuatia mpaka na sisi tumeukuta. Leo nimefika hapa kwa sababu Rais Jakaya Kikwete na wajumbe wenzake wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu walitumia misingi imara iliyowekwa na waasisi wa Chama changu kuamua kuwa nami nina haki ya kuwa Mbunge. Na leo nazungumza hapa nikiamini kuwa ni misingi hiyo hiyo itakayotoa uongozi wa Taifa letu katika awamu ijayo.

Babu yangu mzaa baba aliishi Kijijini Goweko, eneo la Mlimani, na alikuwa mfugaji mkubwa wa ng’ombe na mrina asali mashuhuri. Yeye na mkewe waliishi maisha ya heshima kubwa pale kijijini. Hawakuwahi kusoma wala kuajiriwa japokuwa Babu yangu aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali ndani ya Chama Cha TANU na baadaye CCM katika ngazi ya Kata.

Babu yangu mzaa mama alikuwa mjukuu wa Chifu na hivyo alipata fursa ya kusoma Tabora School miaka miwili mbele ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere. Alifanya kazi mbalimbali chini ya serikali ya wakoloni, na alishiriki harakati za kuanzishwa na kusambaa kwa chama cha TAA na baadaye TANU. Babu yangu aliamini kuwa “binadamu wote ni sawa na kwamba kila mtu anastahili heshima na kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake”, na kwamba ukoloni haukuwa kitu cha sawa, na hivyo kujitawala wenyewe dhidi ya utawala dhalimu wa wazungu ilikuwa ni haki yetu; pia aliamini katika elimu, na hivyo alifanya juhudi kusomesha mabinti zake; mama yangu aliishia kwenye ualimu kabla ya kuingia kwenye ndoa. Babu aliamini kuwa Tanzania ya mabinti zake itahitaji wasomi, ndoto ambayo ninaishi kuitekeleza kwa ajili ya mabinti zangu, Sheila na Hawa, na kaka yao, HK Jr. Ninaamini kila mzazi wa kizazi changu ana ndoto inayofanana na yangu kwa watoto wake.

Ninaamini historia ya maisha yangu siku moja itaandikwa na itawasisimua na kuwapa matumaini makubwa vijana na watoto chini ya miaka 35 ambao ni zaidi ya asilimia 70 ya watanzania wote. Mmoja wa wajukuu zangu ataisoma na kusema ‘doesn’t it get better than this?’

Ninaishi nikiamini kuwa hadithi ya maisha yangu ni mfano hai wa historia ya maisha ya watanzania wengi. Na kwamba, nina deni la kulipa kwa vizazi vijavyo kwa kuwa mimi ninafaidi matunda ya mti uliopandwa na vizazi vilivyonitangulia. Naliona jukumu la kuhakikisha vizazi vijavyo vinafaidi urithi wa Tanzania kuwa ni la kwangu na wenzangu wa kizazi hiki.

Mahusiano ya Watu na Serikali Yao


Kazi yangu imenifikisha sehemu nyingi sana za nchi yetu – vijijini na kwenye majiji, imenikutanisha na watu wa kila aina – matajiri kwa maskini, wazee kwa vijana – hakuna hata mmoja kati ya watu hawa anayetegemea Serikali itamtatulia kero zake zote. Wanajua wanapaswa kufanya kazi kwa bidii ili wasonge mbele – na wana nia ya kufanya hivyo.

Nenda kwa wafanyabiashara wakubwa kule Pugu Road viwandani, kwa matabibu wenzangu pale hospitali ya Taifa Muhimbili, ama kwa wafanyabiashara na wachuuzi pale sokoni Kariakoo, wote watakuambia hawapendi kuona kodi zao zikitafunwa na wachache wasio waadilifu.

Watanzania wanataka kupata huduma bora za afya, elimu, maji, miundombinu.

Nenda kule Nanyumbu, ama Tandahimba, ama kule Nduli, Kyela, wazee kule watakuambia hawategemei Serikali itawaletea ubwabwa kwenye sahani za fedha, wanajua Serikali haitowafanyia kila kitu, lakini wanajua kabisa kuwa wanapaswa kufanya kazi kwa bidii na wamekuwa wakifanya hivyo siku zote. Wanachohitaji wao ni kujengewa mazingira wezeshi kushiriki shughuli zao za kilimo ama biashara, waelekezwe namna ya kuongeza uzalishaji kwa kutumia njia za kisasa za kilimo chenye tija na ufanisi, waelekezwe wanapataje pembejeo, wanapataje mikopo yenye riba nafuu, wanahitaji, mwisho wa siku, wajue wapi watauza mazao yao kwa uhakika na bila kudhulumiwa wala kucheleweshewa malipo.

Watu hawatarajii serikali itabeba mizigo yao yote.   Lakini wanaamini kabisa, kwamba tukibadili kidogo tu vipaumbele vyetu, tukibadili namna tunavyoendesha serikali, tukibadili kidogo namna tunavyoendesha uchumi wetu, tutaweza, kwa kiasi kikubwa, kubadili muelekeo mzima wa maisha ya baadaye ya watoto na wajukuu zetu. Tutaiondoa Tanzania miongoni mwa nchi maskini kabisa duniani.

Na mimi, kama watanzania wenzangu wengi, nina imani kubwa kabisa kwamba, tunaweza kubadili mustakabali wa Taifa letu. Tunaweza kufungua milango ya maisha bora zaidi kwa watanzania. Tutatoa fursa sawa kwa kila mtanzania kuishi kwa matumaini, kwamba atabadili maisha yake wakati wowote ule kuanzia leo. Tutaweza kuamsha ari ya kila mtanzania kuongeza bidii kwenye kazi akitumaini na kuamini kuwa kesho yake itakuwa bora kuliko jana yake, kuwa naye ataishi kwa heshima, raha na starehe ndani ya nyumba yake.

Ninaamini, kutokea ndani kabisa ya mifupa yangu, kuwa tukifanya uchaguzi sahihi wa vipaumbele vyetu, tukibadili namna tunavyoendesha serikali yetu, haya ninayoyasema si ndoto za mchana. Ni mambo yanayowezekana.

Watanzania wengi wanaamini, kuwa tukifanya uchaguzi sahihi wa vipaumbele vyetu, mabadiliko makubwa, na ya haraka yatatokea kwenye uchumi wetu. Wanaamini tukichagua kiongozi sahihi mwakani, anayejua mahitaji ya nchi yetu kwa sasa na baadaye, tutafanikiwa.

Tamko Rasmi la Nia ya Kugombea Urais na Sababu


Ndugu zangu nyote mliopo hapa, natangaza rasmi, kuwa ninatia nia ya kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 2015.

Na nimefikia uamuzi huu bila kuelekezwa, kusukumwa, kushawishiwa, kupangiwa ama kupanga na mtu ama na kikundi cha watu, bali kwa utashi na utayari wangu. Na ninayasema haya, haswa baada ya kutafakari mambo mengi kwa kina: mahitaji ya sasa na baadaye ya Tanzania ya ndoto za kizazi chetu; uwepo wa fursa ya kugombea na kushinda uchaguzi ujao; uwezo wangu wa kuchambua mambo, kutafakari, kufanya maamuzi sahihi, na kuchukua hatua za utekelezaji na kusimamia utekelezaji; uadilifu na uzalendo wangu; na zaidi nia yangu ya kuwa sehemu ya watanzania wengi tunaotaka kuona mapinduzi ya kifikra katika nchi yetu – mapinduzi ambayo yatatia chachu ya mabadiliko ya namna tunavyochagua vipaumbele vyetu kama Taifa na namna tunavyosimamia utekelezaji wa mambo mazuri tunayojipangia.

Ninatangaza nia ya kugombea Urais nikiwapa fursa watanzania wanipime na kunitazama mwenendo na uwezo wangu, nikiamini kabisa kuwa nitapimwa na kuungwa mkono ama kutoungwa mkono, si kwa rangi ya ngozi yangu, si kwa jinsi yangu, si kwa umri wangu, na wala si kwa daraja langu kwenye jamii, ama dini yangu, ama kabila langu. Ninaamini nitapimwa kwa rekodi yangu, sifa, utayari, dhamira na uwezo wangu, kama mtanzania.

Natangaza nia ya kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano ili nipate fursa ya kuukimbiza uchumi wetu kutoka hapa tulipo kwenda mbele zaidi. Mimi ni mwanamabadiliko, ninaamini nikipewa fursa, nitashirikiana na watanzania wenzangu na kwa pamoja tutaunyanyua uchumi wetu kutoka kiwango cha kukua cha tarakimu moja kwenda kile cha tarakimu mbili kwa miaka yote ya uongozi wangu. Ninaamini tutaweza kwa pamoja kuukuza mchango wa kilimo kwenye GDP kutoka asilimia 4.2 kwenda zaidi ya asilimia 6. Tukiyafanya haya naamini tutakuwa tumezalisha ajira nyingi zaidi kuliko leo.

Ninaamini katika Ndoto ya Tanzania. Kuwa leo miaka 50 ya kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuna kila sababu ya kuwa Taifa la dunia ya kwanza, viongozi waliotutangulia wameandaa misingi ya kuifikisha Tanzania kwenye matamanio yetu. Kizazi chetu cha viongozi kina jukumu na wajibu wa kuikimbiza Tanzania kufikia kwenye ahadi inayotokana na ndoto za waasisi wa Taifa letu. Binafsi, niko tayari kulibeba jukumu hilo bila woga wala wasiwasi wowote ule, maana naamini tusipojitokeza watu kama mimi, tutajikuta tunaongozwa na watu wasiostahili. Nina suluhu ya changamoto kubwa za leo na kesho: kupigana na njaa na kuhakikisha usalama wa chakula kwa watu wetu, tatizo la ajira kwa vijana na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi ni miongoni mwa mambo ambayo kizazi chetu kitapaswa kuyafanyia kazi kwa haraka na umakini wa hali ya juu. 

Na ndugu watanzania wenzangu, amini nawaambia, kuwa tuna kazi ya ziada ya kufanya mbele yetu. Kazi ambayo ninaamini tunaiweza tukiamua; uwezo tunao, sababu tunazo na nia tunayo – sema tuna mapungufu makubwa kwenye kuchukua hatua za kutenda.

Kutathmini na Kuwapima Watia Nia


Nyote mliopo hapa na wanaotusikiliza kutokea nje ya hapa mna jukumu la kututazama kwa ukaribu sana, kututathmini na kutupima sote; tuliojitokeza hadharani, walioanza safari za matumaini, wanaotajwa tajwa, na wale wanaosubiri kuoteshwa, ili wakati muafaka ukifika muwape taarifa sahihi watanzania, kuwa kati yetu sote, ni nani anafaa kuliongoza Taifa hili kuelekea Tanzania ya ndoto zetu!

Kuwa, ni nani kati yetu ataweza kuwa Amiri-jeshi-mkuu, siyo kwa uanajeshi wake bali kwa uwezo na utayari wake wa kuwashirikisha wataalamu wa majeshi na kuamua kwa busara kutumia nguvu za kijeshi pale inapolazimika baada ya kupima na kuchambua aina nyingine zote za kutafuta suluhu za migogoro kabla ya kuamua vita.

Kuwa, ni nani kati yetu anayeamini katika uhuru, haki na usawa na wajibu wa watu wote, kama unavyolindwa na Katiba yetu, pia asili na historia yetu, anayeamini katika haki ya kuabudu lakini asiyekuwa tayari kuitumia haki hiyo kuwagawa watanzania kutokana na dini zao.

Kuwa, ni nani kati yetu anayeamini katika Haki ya kupata huduma bora za afya, elimu, maji, kama wanavyopata wabunge na mawaziri wetu, kama wanavyopata mahakimu na majaji wetu, kama wanavyopata wafanyabiashara na wakurugenzi wetu.

Kuwa, ni nani kati yetu ataweza kuhakikisha kuwa watanzania wote wanapata haki hizi bila kutazama hali zao kiuchumi ama daraja zao kijamii.

Kuwa, ni nani kati yetu ataweza kuhakikisha kila mtanzania ana bima ya afya na ya maisha, na kwamba bima hiyo inampatia uhakika wa kupata huduma bora za afya popote na kwa wakati anapozihitaji bila kumbagua kwa hali yake. Kwamba, itakuwa mwisho sasa, ndani ya hospitali moja, kuwa na wodi nzuri wanazolazwa ‘wateule wachache waliochangia bima ya afya’ na kuwa na wodi za ‘ilimradi’ tu wanazolazwa wengine.

Kuwa, ni nani kati yetu anaamini zaidi katika uhuru na kujitegemea kwenye masoko na malighafi ili kudhibiti uchumi wetu mpana wa ndani, kujitegemea kwenye masoko ya pamba na nguo, kwenye mafuta ya kula, kwenye chakula cha uhakika kwa ajili ya watu wetu, kwenye mafuta na gesi ili tukwepe mtego wa kuwa sehemu ya uchumi, masoko na biashara za hasara na faida za makampuni makubwa ya kimataifa nje ya mipaka yetu. Ili tulinde thamani ya fedha yetu, ili tuwe na uhakika wa ustawi wa maisha ya watu wetu ndani ya nchi bila athari kubwa kutoka nje ya nchi yetu?

Kuwa, ni nani kati yetu anaichukia rushwa, anachukia wakwepa kodi wa makampuni makubwa ya kimataifa yanayovuna raslimali za nchi yetu na hayalipi hata kodi tu! Kwamba, ni nani atalinda raslimali za nchi yetu bila shaka. Kwamba, ni nani kati yetu atahakikisha tunapata hisa za kutosha kutokana na uchumi wa raslimali za madini, vito, mafuta na gesi? Kwamba, ni nani kati yetu atailinda ardhi ya watanzania na kuhakikisha haivamiwi na wasaka ardhi kutoka nje ya Taifa letu, kwamba atahakikisha ardhi inabaki kutumiwa kwa faida ya wakulima na wafanyakazi wa nchi yetu?

Kuwa, ni nani kati yetu ataweza kupambana na changamoto za usafiri na usafirishaji, kuwa ataweza kuongeza tija na ufanisi kwenye bandari zetu, na ataweza kufufua usafiri wa reli, ndege na meli?

Kuwa, ni nani miongoni mwetu anaakisi taswira sahihi zaidi ya watanzania walio wengi, historia yake, rekodi yake, wajihi wake, mtazamo wake, ndoto zake, zinaakisi ‘utanzania’ halisi. Kuwa, yeye ni hitaji sahihi la watanzania?

Wakati ukifika, muwaeleze watanzania ukweli, wafanye uamuzi unaotokana na taarifa sahihi, wachague mtu sahihi. Mtu ambaye ukimtazama kwa nje ana mvuto na analeta matumaini kwa watanzania, ambaye ukimcheki hivi unasema ‘he is just a cool guy’, lakini kwa ndani anaumia, anaungua moyo wake kwa ajili ya Tanzania yetu.

E Pluribus Unum


Mimi naamini kwamba; E Pluribus unum. Baina ya wengi, mmoja!

Kwamba; Mimi ni mmoja kati ya uwingi wetu. Siwezi kuwa salama kama wengine hawako salama, siwezi kuwa na raha kama wengine wanateseka. Ninaongozwa na ile dhana kwamba, matatizo ya mwenzangu, ni ya kwangu pia, na haiishii hapo tu, matatizo hayo si yangu na huyo mwenzangu tu, ni yetu sote kama jamii.

Hivyo:

kitisho cha njaa ya familia fulani maskini kule Sakasaka, wilayani Meatu, ni kitisho changu na familia yangu.

Kucheleweshewa haki ya kuhukumiwa kwa mtuhumiwa wa mauaji ya kule Sombetini, Arusha, ni kitisho kwangu pia, hata kama kesi siyo yangu.

Mzee Makame wa kule Wete, Pemba, aliyefiwa na watoto wake akakosa msaada na yeye hana nguvu za kuzalisha tena, anavyokula mlo mmoja kwa siku ili asukume siku, inaniumiza na kunigusa moyoni, hata kama yeye siyo babu yangu.

Mama John ni mpishi mzuri wa wali nazi kwa maharage, na ana wateja wengi mtaani kwake maeneo ya Mtaa wa Sikukuu, Kariakoo; akifukuzwa, akapigwa virungu, akanyang’anywa pesa zake, akadhalilishwa na kumwagiwa chakula chake na mgambo wa jiji la Dar es salaam kwa kuwa anafanya biashara mahala pasiporuhusiwa, inaniumiza na kunigusa moyoni, hata kama yeye si mama yangu.

Kama kuna mtoto asiyejua kusoma na kuandika kule Mrijo Chini, hiyo inaniuma na kunigusa sana moyoni, hata kama yeye si mwanangu.

Kato na Kokugonza ni wanandoa wapya, wanaishi kijijini kule pembezoni ya Katerero, Koku amepata ujauzito na amefikia kujifungua, kwa hali yake na namna mtoto alivyokaa tumboni anapaswa akajifungulie hospitali ya wilaya ili ikibidi kufanyiwa operesheni, basi afanyiwe; ikitokea uchungu umeanza ghafla na akachelewa kufika hospitali ya wilaya sababu ya miundombinu mibovu na kukosa ambulance mapema, akapoteza damu nyingi hadi umauti ukamkuta yeye na mwanae, ni jambo lenye kuuma sana, si tu kwa Kato na wanafamilia wao, bali na mimi pia linaniuma na kunigusa sana moyoni, hata kama yeye si mdogo wangu.

Bwana Kalumanzila ni mmachinga wa nguo za mitumba mitaani. Yeye huchukua nguo zake kumi kwa kuaminiwa na mwenye belo kutokea soko la Karume, akiuza anachukua kifaida kidogo kinachozidi hapo juu na kurudisha pesa ya mwenye mali Karume jioni ya siku hiyo. Elfu mbili ama tatu anayopata inamfanya aishi yeye na mkewe na watoto wake. Akifukuzwa barabarani na akanyang’anywa mali, anakosa kazi ya kufanya na analazimika kumtumikia bosi mwenye mali mpaka atakapofidia mali iliyopotea bila kupata cha juu. Shida na madhila anayoyapata bwana Kalumanzila zinaniumiza na kunigusa sana moyoni, hata kama yeye si mjomba wangu.

Fikra hizi zinatokana, kwa kiasi kikubwa, na funzo nililopewa na babu yangu wakati nikichagua kozi ya kusoma chuo kikuu, ambapo nilipata kitendawili cha kuchagua kati ya kwenda kusoma udaktari ama sheria; aliniambia kuwa, “ni bora ukachagua kusoma udaktari maana utapata baraka za Mungu kwa kujitoa kuwasaidia watu walio na shida…” na akaendelea kusema kuwa “…kwenye maisha yako ikitokea ukapata mali ama ukawa na nafasi kubwa ya kuamua juu ya mustakabali wa maisha ya wengine, usisahau kumshukuru Mungu kwa kuwatendea yaliyo mema wenzako na Mungu atazidisha Baraka zake kwako.” Leo miaka zaidi ya 15 baadaye naona maneno yake bado yanaishi moyoni mwangu. Maisha yangu yote nimeikumbatia falsafa hii. Nimeifanya kuwa dira ya utumishi wangu kwa wenzangu na kwa ulimwengu.

Falsafa hii imenifanya nishindwe kuvumilia unyonyaji, ukandamizaji, uzembe, wizi na ubadhirifu wa baadhi ya wenzetu walioshindwa kudumu kwenye njia ya kutoa haki, uadilifu, uwajibikaji na utumishi uliotukuka.

Tamati


Ndugu wanahabari, Tarehe 4, Agosti 2014, Rais Kikwete akihutubia kwenye Kituo cha Maendeleo ya Dunia (Center for Global Development) alisema: “…Nataka na natamani kuwa Rais wa mwisho wa Tanzania kuongoza nchi masikini. Raslimali ya gesi inatoa nafasi na fursa kubwa kwa nchi yetu kuondokana na umasikini. Mimi nimeongoza nchi masikini, lakini nataka mrithi wangu kuongoza nchi yenye ustawi na utajiri…” Mimi nasema hivi: nataka na natamani kuwa Rais wa kwanza wa Tanzania kuongoza nchi Tajiri. Kama nitafanikiwa kuwa Rais, nitatumia miaka ya awali ya uongozi wangu kuikimbiza Tanzania kuelekea kwenye ndoto hii.  

Kuna watu wanadhani uwepo wa mfumo wa demokrasia imara, ama mfumo unaotoa uhuru na haki kwa watu wetu, ama uwepo wa mfumo wa soko huria, ama utandawazi ni muarobaini wa kudumisha amani yetu, mimi nasema, tunahitaji zaidi ya uhuru, zaidi ya demokrasia, zaidi ya mifumo ya utandawazi, ama ya soko huria ili tudumishe amani na mshikamano wetu – tunahitaji uhuru kwenye uchumi wetu. Tunahitaji uhuru kwenye mifuko ya kila mtanzania. Uhuru wa kuchagua anachotaka kula, kuvaa ama huduma kwa ajili yake na familia yake. Tunahitaji mabadiliko ya kifikra ili kuleta mapinduzi ya uchumi tunayoyatarajia. Tunahitaji kupigana kuhakikisha kila mtanzania anajitegemea kiuchumi. Hapo ndipo tutasema sasa tuna uhuru kamili.

Mungu awabariki sana. Mungu ibariki Tanzania. Mungu ibariki Afrika.


MATUKIO-MICHUZI: Dk. Kigwangala aitaka TAMISEMI kuwashirikisha Wananchi kubuni Vyanzo vya Mapato

Wednesday, May 7, 2014
MATUKIO-MICHUZI: Dk. Kigwangala aitaka TAMISEMI kuwashirikisha Wananchi kubuni Vyanzo vya Mapato

MATUKIO-MICHUZI: Dk. Kigwangala aitaka TAMISEMI kuwashirikisha Wananchi kubuni Vyanzo vya Mapato

MATUKIO-MICHUZI: Dk. Kigwangala aitaka TAMISEMI kuwashirikisha Wananchi kubuni Vyanzo vya Mapato

Hawa Siasa Kigwangalla's Tennis Training

Sunday, March 9, 2014