MSIMAMO WA MBUNGE WA NZEGA KUHUSU POSHO

Monday, December 12, 2011
Kufuatia kuwepo kwa mjadala mzito wa kitaifa kuhusu ongezeko la posho ya kikao (Sitting allowance) ya wabunge kama ilivyoongezwa siku za karibuni, ofisi ya Mbunge wa Nzega imelitafakari suala hili na kuona umuhimu wa kutoa taarifa kwa wananchi wa jimbo la Nzega na watanzania kwa ujumla kuhusiana na msimamo wa Mhe. Mbunge. Tamko hili linazingatia maswali mengi kutoka kwa wapiga kura wa jimbo la Nzega na baadhi ya watanzania waliotaka kujua nini msimamo wa Dr. Hamisi Kigwangalla, MB (Nzega, CCM) kuhusu posho, hususan ongezeko hili la kutoka 70,000 hadi 200,000.

Mbunge wa Nzega ana msimamo ufuatao:

Kwamba, posho ama ujira wa mwia, ni malipo halali ya kazi ya Mbunge na kwamba ongezeko lolote litakalofuata kanuni na taratibu za haki na usawa kwa watu wote litakuwa halali.

Kwamba, Ongezeko hili kama lilivyotamkwa na Mhe. Spika Anna Makinda (MB), limekuja kutokana na ongezeko la ukali wa maisha katika mji wa Dodoma linaleta mashaka na utata mkubwa kuhusiana na uhalali wake, linaonesha usaliti wa wabunge kwa wananchi waliowachagua na linaiaibisha taasisi ya Bunge kama mtetezi wa wanyonge na mdhibiti na msimamizi mkuu wa serikali. Mbunge wa Nzega anaamini kwamba sababu hii inawakimbiza wabunge mbali zaidi na wananchi na kwamba ni kweli kuna mfumuko mkubwa wa bei lakini hauwagusi wabunge tu pekee yao, unamgusa kila mtanzania, na kama ofisi ya Rais inaona umuhimu wa kuboresha hali ya maisha ya wabunge, basi ingewapandishia mishahara yao, ingewaongezea mafuta ya gari kwa ajili ya kufanyia kazi zao, ingeboresha mfuko wa jimbo, ingeboresha ofisi zao n.k. Kwa hakika kabisa, kwa sababu zilizotolewa na Mhe. Spika, posho iliyopaswa kuongezwa siyo posho ya kikao bali ni posho ya kujikimu. Na hata kama Mhe. Spika alikuwa na nia ya kuongeza posho ya kikao, basi kwa vyovyote vile sababu isingekuwa hii ya ukali wa maisha mjini Dodoma, maana hauongezeki kwa wabunge peke yao tu!

Kwamba, kwa kuwa sababu za kuongezwa kwa posho ya kikao haziendani na malengo ya uwepo wa posho hiyo, basi wabunge wote waungane mkono na Mbunge wa Kigoma Kaskazini Mhe. Zitto Kabwe, Mbunge wa Bumbuli Mhe. January Makamba na Mbunge wa Nzega Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla (Nzega) waikatae posho hii ili kuwatendea haki watanzania wanaohangaika kutafuta mkate wao wa kila siku. Kuna madaktari wanakesha usiku kucha na wanalipwa posho ya on call allowance ya TZS 10,000 tu, kumlipa Mbunge posho ya 200,000 haijengi mazingira ya usawa ya kuugawana umaskini wa nchi yetu.

Kwamba, ili kupunguza visingizio vya wabunge kudai maslahi makubwa zaidi kwa kuwa wanaombwa sana amisaada na wapiga kura wao, ofisi ya Bunge ianzishe kitengo cha kutoa elimu kwa umma kuhusu kazi na majukumu ya Mbunge ili kuwaelimisha wananchi kwamba kusaidia matatizo binafsi siyo kazi yao na hivyo wasihukumiwe kwa kutokutoa misaada bali kwa kuisimamia serikali ipasavyo.


Tamko hili limetolewa leo Tar 12/12/2011 na Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Nzega, Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla (MB).

Mapinduzi ya Kijani (Pamba) Yamefanikiwa Nzega!

Tuesday, November 8, 2011
Katika hali ya kutia moyo, wilaya ya Nzega imefanikiwa kufufua kilimo cha Pamba. Zao hili la biashara lililokuwa limepotea kabisa wilayani hapa sasa limerudi upya tena, japokuwa si kwa kufikia kiwango cha zamani lakini mwanga wa matumaini unaangaza kila kona. Wilaya ya Nzega iliacha kulima pamba takriban miaka 12 iliyopita kufuatia kuanguka kwa utaratibu mbovu wa ushirika uliokuwepo. Tatizo hili halikuikumba Nzega peke yake bali ukanda wote wa Western Cotton Growing Area (WCGA) (yaani mikoa ya Tabora, Shinyanga, Mwanza, Mara, Kigoma, Singida, Kagera n.k). Ushirika ulikuwa ukinunua pamba kwa mkopo na kulipa wakulima pesa yao kwa awamu. Mwaka 1990 wakulima wote hawakulipwa pesa ya malipo yao ya awamu ya pili. Hii iliwakatisha sana tamaa na wengi wao waliacha kulima pamba msimu wa kilimo uliofuatia. Mwaka 1991, bei za pamba zilizidi kuanguka kwenye soko la dunia na hivyo kusababisha ushirika tena kushindwa kununua pamba ya wakulima vizuri ipasavyo, na mzunguuko huu ulipelekea wakulima wengi zaidi kususa kulima pamba misimu iliyofuatia. Mfumo wa masoko ulipoboreshwa kwa kuingia kwa soko huria hapo baadaye, sehemu nyingine zilirudia kilimo cha pamba lakini Nzega ilikoma kabisa na pamba ikabaki historia! Na huu ulikuwa mwanzo wa kushamiri wa kwa umaskini wilayani Nzega. Maana wakulima walilazimika kuuza chakula ili wapate hela badala ya kuuza mazao ya biashara.

Kampuni ya MSK Solutions Ltd ikishirikiana na Serikali wilaya ya Nzega na Kampuni ya Rural Livelihood Development Company (RLDC) wamejifunga mikanda na kwa pamoja wamefanikiwa kuleta mapinduzi ya ukweli ya kijani. Pamba imerudi tena Nzega, imerudi kwa kasi ya ajabu ambayo haikutegemewa. Kwa pamoja wadau hawa wamekuwa wakiendesha mradi wa Nzega Cotton Development Project (NZECODEP) ambao unafadhiliwa kwa pamoja na wadau wawili, MSK Solutions Ltd na RLDC.

Mradi huu umeweza kufanikiwa kwa sababu zifuatazo, kwanza umewahakikishia wakulima soko la uhakika na bei nzuri zaidi ya pamba yao. Pili, mradi unahakikisha upatikanaji wa pembejeo na zana za kilimo cha pamba karibu na wakulima na kwa bei nzuri zaidi. Tatu, wakulima wanahakikishiwa ushauri wa kitaalamu karibu zaidi kwa kuwa mradi unawawezesha posho kidogo mabwana shamba ili kuwatia morali zaidi wa kutoa huduma za ugani.

Katika uhamasishaji huu, ujumbe mahsusi unaowafikia wakulima ni pamoja na uhakika wa vitu vyote hivi na pia maelezo yanayotoa cost-benefit analysis ya kilimo cha pamba ukilinganisha na mazao mengine na kwamba pamba haikuja kufuta kilimo cha mazao mengine bali kuhakikisha mkulima anakuwa na zao la mbadala endapo ikitokea amekosa mavuno ya kutosha ya mazao ya chakula ama mengine ya biashara atakayokuwa amelima. Pia wakulima wanaeleimishwa kuwa pamba inastahimili ukame ukilinganisha na mahindi na mpunga na hivyo kama mkulima akikosa hayo mazao mengine yote na akapata pamba, atauza atapata hela na kwenda kununua chakula. Na kama akipata mazao mengine, basi atafanya mambo mengine kwa kutumia hela itokanayo na pamba.

Kutoka kilo 20,000 Mwaka wa Kwanza, hadi 350,000 na sasa Kilo 982,000! Mbali na kukuza kipato cha mkulima mmoja mmoja, pamba itakuwa ni chanzo kipya kikubwa cha mapato ya halmashauri ya wilaya ya Nzega kupitia ushuru wa mazao (district cess) na hivyo kufanikisha miradi mbali ya maendeleo kama mabarabara, shule, zahanati n.k. Pia faida nyingine ni pamoja na kuongeza mzunguko wa fedha na hivyo kutia chachu sekta nyingine za maendeleo na huduma wilayani hapa. Pia kushamiri kutaleta viwanda wilayani hapa. Maendeleo haya ni endelevu na yanagusa watu wengi ukilinganisha na uwepo wa mgodi mkubwa wa uchimbali dhahabu ambapo ikiisha ndiyo basi tena.

Kikwazo kikubwa kinachoukumba mradi, pamoja na mambo mengine, ni propaganda za kisiasa zinazofanywa na wanasiasa kwa vile tu harakati za kufufua zao la pamba Nzega zinafanywa na kampuni ya MSK Solutions Ltd ambamo Mbunge wa Jimbo la Nzega ana hisa.


Makala hii imeandaliwa na Ndg. Kumotola L. Kumotola, Afisa Mahusiano, Uratibu na Itifaki - Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Nzega akishirikiana na Ndg. Hassan Jaha, Mratibu wa Mradi wa NZECODEP, MSK Solutions Ltd, Nzega.

Volunteers at Work!

Volunteers at Work!

Monday, November 7, 2011

Are we Realistically Trying to Solve the Electricity Problem in Our Country?

Tuesday, June 7, 2011
Mpaka leo hii, tuna mitambo ya jumla ya MW 336 inayowashwa kwa kutumia gesi asilia, yaani kuna ile inayomilikiwa na kuendeshwa na Songas (MW 191), ile ya serikali ya Ubungo (MW 100) na ile ya Tegeta (MW 45). Hii mitambo tu ukiongeza na ile ya makampuni kama matatu hivi yanayotumia gesi asilia kuendeshea mitambo yao, yameisha-exhaust supply ya gesi. Hata ile ya Dowans ikiwashwa leo, bado haitoweza kuwaka to full capacity (ya 112 MW), badala yake itazalisha MW 75 tu, kwa sababu ya poor supply ya gesi.

Leo hii kuna miradi ya Ubungo - MW 100, Kinyerezi MW 260 na Somanga Fungo MW 240, jumla yake ni MW 600. Je, serikali iko tayari kuwekeza kwenye bomba jipya litakalosaidia kutatua tatizo hili la upatikanaji wa gesi, ambalo ni very expensive?

Leo hii serikali inalalamikia gharama za uendeshaji wa mitambo ya IPTL, inayotumia Heavy Fuel Oil (HFO) kuwa ziko juu sana, sasa kwa nini tena inajenga power plant ya Mwanza (MW 60) kwa mitambo itakayotumia HFO ilhali wanaiona IPTL inavyosumbua kwa gharama?

Saa nyingine unashindwa kuelewa ni jinsi gani wasomi wetu wanafanya maamuzi mazito kama haya! Sijui wanakuwa wanatumia vigezo gani?

Hivi kwa nini serikali isianzishe mradi wa Umeme na wakajikita zaidi kwenye MW chache tu zilizo ndani ya uwezo wetu? Kama walivyofanya kwenye barabara kwa nini wasifanye hivyo pia kwenye umeme???

TATIZO LA UMEME NCHINI!

Mhe. Dkt. Hamisi Andrea Kigwangalla (MB), atauliza:-

(a) Tangu serikali ya awamu ya pili hadi leo, serikali imetumia jumla ya shilingi ngapi kuzalisha umeme, na bado tatizo lipo?

(b) Je, tatizo la umeme nchini litaisha lini?

(c) Kwa nini serikali inaongea mipango mingi ya kutatua tatizo la umeme bila kutekeleza na kwa nini suala la upatikanaji umeme nchini ni la dharura kila siku?

Waziri wa nishati na madini atajibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hamisi Andrea Kigwangalla, Mbunge wa Nzega lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mhe. Spika, uwekezaji wa serikali katika miradi ya kuzalisha umeme tangu kipindi cha serikali ya awamu ya pili hadi leo unafikia jumla ya Dola za Marekani milioni 798.

(b) Mhe. Spika, tatizo la uhaba wa umeme litaisha baada ya kutekeleza kwa ukamilifu na kwa wakati mpango wa kipindi kifupi cha 2011 - 2015 kama ilivyofafanuliwa kwenye mpango kabambe wa uendelezaji wa sekta ya umeme wa mwaka 2009. Miradi itakayotekelezwa kipindi hicho itaongeza jumla ya MW 1830 kwenye mfumo wa gridi ya Taifa kwa gharama inayokadiriwa ya Dola za marekani milioni 3,700.

(c) Mhe. Spika, serikali imeazimia kutekeleza kwa wakati miradi ya kuzalisha na kusafirisha umeme kulingana na Mpango Kabambe wa Uendelezaji wa sekta ya Umeme, hususan, katika kipindi cha 2011 - 2018. Miradi iliyopangwa kujengwa itaongeza MW 600 kwa kutumia maporomoko ya nguvu za maji, MW 870 kwa kutumia gesi asili, MW 1200 kwa kutumia makaa ya mawe na MW 100 kwa kutumia nguvu ya upepo. Serikali inategemea miradi hii itakamilika kwa kushirikisha uwekezaji wa sekta binafsi kwa kuwa gharama za miradi hii yote ni kubwa.

Mhe. Spika, serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi imeanza mikakati ya kutafuta fedha za kugharamia miradi ya kipaumbele niliyoitaja hapo juu.

Maswali Mawili ya Nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Kigwangalla:

(1) Kama toka awamu ya pili mpaka leo hii serikali ilitumia Dola za Marekani milioni 798 na bado hali ya upatikanaji umeme nchini ni duni kiasi hiki, serikali hii leo itapata wapi Dola za Marekani milioni 3,700?

(2) Mpaka leo miundombinu ya kusafirisha gesi kutoka Mnazi bay na Songosongo kwa ajili kuzalishia umeme kwenye mitambo iliyopo Dar es salaam ni duni na imechakaa, na uwekezaji kwenye bomba la kusafirishia gesi ni gharama kubwa, mnatuhakikishiaje dhamira ya serikali ya kulitatua tatizo la umeme kwa haraka kwamba ni ya ukweli au tutegemee kuendelea kufaidi mgao kila siku?

Kada Kigwangalla Akicheza Ngoma na Wanachama Wenzake wa CCM!

Tuesday, May 10, 2011
CCM bwana, raha tupu! I am so proud to be a member of the CCM party!

Mwaliko wa Maandamano Kupinga Uwepo wa Mgodi wa Golden Pride Project Nzega!

Monday, March 7, 2011
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Nzega inakualika kwenye Maandamano ya Amani kupinga uwepo wa Mgodi wa Kuchimba dhahabu wa Golden Pride Project, Nzega, kwa kuwa hauna faida kwa Nzega na kwa Taifa, Unaharibu mazingira, Umegubikwa na usiri mkubwa, Wachimbaji wadogo na wakazi wa maeneo mgodi huu ulipo hawajalipwa fidia mpaka leo, wananchi wa Nzega hawapati fursa za ajira wala tenda mbalimbali mgodini humo, unatumia maji mengi zaidi ya wenyeji, unachafua na kuharibu vyanzo vya maji, uongozi na wamiliki wa mgodi hawana ubinadamu na huruma kwa wenyeji wa Nzega na hata nchi yetu kwa ujumla n.k. Maandamano haya yatafanyika mnamo Tarehe 3/4/2011 Mjini Nzega. Muda wa kuanza, mahali pa kukusanyikia/kuanzia na kumalizia mtatangaziwa. Nyote mnakaribishwa kuunga mkono jitihada hizi za kudhibiti wizi wa Raslimali za Taifa na uharibifu mkubwa unaofanyika!